Friday, September 14, 2018

RC Ally Hapi Awafunda Vijana wa JKT Mafinga

Mkuu wa Mkoa Iringa Mhe Ally Salum Hapi akikagua gwaride la Vijana wa JKT Mujibu wa Sheria Operesheni Mererani Wakati akifunga Mafunzo hayo katika kikosi cha Jeshi Mafinga (Picha na Amani Mbwaga)
Na Amani Mbwaga, Mafinga

Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe Ally Salum Hapi akiwa Mgeni Rasmi Leo amefunga mafunzo ya awali ya kijeshi kwa vijana wa Mujibu wa Sheria 2018 Oparesheni Mererani katika Kikosi cha Jeshi Mafinga JKT Kilichopo Wilayani Mufindi Mkoani Iringa.

Hapi amewataka vijana kufanya kazi kwa bidii, kuepuka vitendo vyote viovu, kukemea rushwa, uvivu usaliti, ukosefu wa maadili na uvunjaji wa sheria za nchi.

“Serikali yetu chini ya Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli inathamini na kutambua mchango wa vijana katika Taifa hili na ndio maana imeendelea kugharamia mafunzo yenu kwa kila namna hivyo kwa pamoja tunakila sababu ya kuipongeza serikali yetu kwa kutambua juhudi hizi, ni imani yetu kwamba mtatuunga mkono katika ujenzi wa Tanzania ya Viwanda” alisema Mhe Hapi

Amewasihi vijana kwenda kuishi kwa mujibu wa kiapo walichoapa, wakawe mfano kwa vijana wengine ili waige mema waliyojifunza ikwemo kuwa na nidhamu ya kijeshi katika maisha yao na kuzingatia mambo makuu matatu kwa mwanajeshi ambayo ni Uaminifu, Utii, na Uhodari katika kufanya kazi na kulinda rasilimali za Taifa.

Mafunzo ya awali ya kijeshi kwa vijana wa mujibu wa sheria Oparesheni Mererani yalifunguliwa rasmi na aliyekuwa Kamanda Kikosi Kanali Hamis Maiga mnamo tarehe 25 Juni 2018 kukiwa na vijana 1438 kati yao wasichana idadi 363 na wavulana idadi 1075.

Mpaka leo vijana waliomaliza mafunzo idadi ni 1416 wavulana wakiwa idadi 1055 na wasichana 361 baada ya vijana 20 kati yao vijana 19 ambao ni wavulana na msichana 01 kuacha mafunzo kwa sababu ya utoro na vijana 02 kupata uhamisho kwenda Ruvu JKT.

Katika kipindi chote cha mafunzo vijana hawa wamejifunza mambo mbalimbali ikiwemo masomo ya nadharia ambayo yalijumuisha masomo ya uraia, mbinu za kivita na afya.

Pia wamefundishwa mafunzo ya vitendo ikiwemo utimamu wa mwili, mafunzo ya porini, kwata na stadi za kazi ikiwemo kilimo, ufugaji na utunzaji wa mazingira.
Aidha Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri William alisema Wilaya ya Mufindi inanufaika sana na uwepo wa Kikosi cha Jeshi Mafinga na vijana hao kuwepo kikosini kwani toka wamefika hajawahi kupata taarifa yoyote mbaya kuhusiana na utendaji wao wa kazi.

“Vijana hawa wamekuwa mfano wa kuigwa na jamii yetu inayowazunguka na mufindi kwa ujumla hivyo ninawaomba mkawe mabalozi wazuri kwa kuitangaza vyema wilaya yetu Mufindi, Mkoa wetu wa Iringa na Tanzania kwa Ujumla” alisema Mhe William.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkuu wa JKT Kanali Ahmed Abas Ahmed ambaye anamuwakilisha Mkuu wa JKT Meja Jenerali Martin Busungu alisema waasisi wa taifa hili waliona umuhimu kwa vijana wa Tanzania kupata malezi yanayoendana na misingi ya Taifa letu ndipo wakaaamua kuanzisha chombo hiki JKT kitakachowalea vijana ili waendane na desturi na utamaduni wa Taifa letu.

“Pamoja na jukumu hilo la msingi la Jeshi la Kujenga Taifa liliongezewa majukumu ya uzalishaji mali na ulinzi, majukumu hayo matatu yanalenga kuwaandaa vijana kuwa na moyo wa uzalendo na kupenda kazi za mikono, kijutuma, kulinda na kutetea nchi yetu” alisema Kanali Ahmed.

Naye Mkuu wa Kikosi cha JKT Mafinga Luteni Kanali Issa Daud Chalamila alieleza baadhi ya changamoto zilizojitokeza katoka mafunzo hayo ya Vijana wa mujibu wa Sheria 2018 ikiwemo Vijana kuchelewa kuripoti vikosini kwa ajili ya kuanza mafunzo kwa wakati baada ya kuchaguliwa kujiunga na JKT, Muda wa mafunzo kuwa mfupi, kuingiliwa kwa ratiba za udahili wa vyuo vikuu na uombaji wa mikopo ya elimu ya juu ambapo hupelekea kusimamishwa kwa kozi kwa takribani wiki mbili, changamoto zingine ziligeuzwa kuwa fursa.

Luteni Kanali Chalamila akitoa nasaha kwa vijana alisema “Vijana wetu mnaomaliza leo mafunzo haya naomba niwakumbushe kuwa ninyi ni miongoni mwa vijana wachache mliopata fursa ya kufanya mafunzo ya JKT, kupitia kodi za wananchi, serikali  imegharamia mafunzo yenu  hivyo mnalo deni la kulipa, mkawe wazalendo wa kweli kwa Taifa lenu na kuiunga mkono serikali kwa kufanya kazi kwa bidii ili kuleta maendeleo kwa kuzingatia sera ya Hapa kazi tu na pia muwe chachu ya mabadiliko chanya yenye kuleta tija na ufanisi katika jamii ya Tanzania kuelekea Tanzania ya Viwanda”.

JKT ilianzishwa Julai 10, 1963 katika uwanja wa ndani wa Michezo wa Taifa (Indoor Stadium) Majira ya saa Kumi Jioni ambapo viana 11 wakiwa makatibu wa Tanzania Youth League (TYL) walijiunga kwa mafunzo katika kambi ya JKT Mgulani Jijini Dar es salaam.

Katika uzinduzi huo Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere alihutubia taifa akisema kuwa “umuhimu wa JKT ni Taifa kuhitaji huduma ya vijana kulitumikia Taifa lao katika majukumu mbalimbali yatakayotolewa ama kujitokeza kijamii, kiuchumi, kielimu na kiitikadi”

Sanjari na hilo mwaka 1964 ilitungwa sheria ya JKT (National Service Act) ambayo ilimpa madaraka Mkurugenzi wa JKT Kuandikisha vijana wa kujitolea kujiunga na Mafunzo.

Sheria hiyo ilifanyiwa marekebisho mwaka 1966 na 1967 ili kuwezesha vijana waliokuwa wakihitimu elimu ya sekondari ya kidato cha nne na sita kujiunga JKT Kwa mujibu wa sheria.

Kufuatia marekebisho hayo kulitoa fursa kwa kundi la vijana 11 kujiunga na JKT Kwa mujibu wa sheria ambao walitawanywa katika vikosi mbalimbali vya mafunzo.

Baadhi ya Vijana hao ni aliyekuwa Rais wa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) na Makamu wa kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania marehemu mzee Aboud Jumbe, Makamu wa kwanza wa Rais na Waziri mkuu Marehemu Rashid  Kawawa na Spika wa Bunge Hayati Chifu Adamu Sapi Mkwawa wakiwa operesheni    Kazi “A”

Mwaka 1975 JKT Iliunganishwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) ambapo majukumu yake ya malezi kwa vijana na uzalishaji mali na ulinzi wa Taifa yalibaki katika taasisi hiyo, hivyo ilikuwa Kamandi ya Uzalishaji mali ya Jeshi.

Mafunzo ya JKT kwa vijana wa Kujitolea na mujibu wa sheria yaliendelea kwa ufanisi mpaka mwaka 1994 serikali ilipositisha kwa sababu mbalimbali za kiuchumi.

Kusitishwa kwake watafiti walisema kuwa jamii ilishuhudia mmomonyoko mkubwa wa maadili na uwajibikaji usiozingatia nidhamu hasa kada ya vijana.

Mmmomonyoko huo ulizusha malalamiko ya Makundi mbalimbali ya jamii yakitaka kurejeshwa kwa taasisi hiyo hali iliyowezeshwa na serikali ya Awamu ya tatu chini ya Rais na Amiri Jeshi mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Benjamini William Mkapa kuyahisha mwaka 2001 kwa vijana wa kujitolea.

Mnamo Machi 26 mwaka 2013 serikali ya Awamu ya nne chini ya Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Mjeshi ya Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Kikwete Alizindua upya mpango wa Mafunzo ya JKT kwa vijana wa Mujibu wa Sheria.

JKT inachangia sana kuimarika kwa umoja wa kitaifa ambapo vijana wengi wanaohitimu mafunzo haya wanapenda kufanya kazi za mikono kwa moyo, kujituma, kujitolea ujasiri, uvumilivu, ushirikiano na nidhamu.

Aidha Mnamo Machi 15 mwaka 1967 Kikosi cha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Mafinga   kilianzishwa baada ya Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya ulinzi na Usalama wa awamu ya kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere kukabidhiwa shamba lililokuwa likimilikiwa na Kabaila wa Kizungu Bwana Lord Cheseum, litumike kwa mafunzo ya vijana, Ufugaji na Kilimo.

Mkuu wa Kikosi wa Kwanza alikuwa ni Senior Master EP Njau aliyeweza kutekeleza majukumu yake kwa weledi, uadilifu, uaminifu na nidhamu ya hali ya juu ya malezi ya vijana na miradi ya uzalishaji mali.

Mkuu wa Mkoa Iringa Mhe Ally Hapi Akipokea Salamu ya Heshima





Mkuu Wa Mkoa Iringa Mhe Ally Hapi akikagua Kikundi cha Brass Band cha Mafinga JKT Wakati wa Mahafali ya Vijana hao yaliyofanyika leo 





Mkuu wa Mkoa Iringa Mhe Ally Hapi Akiteta jambo na Kamanda Kikosi wa Mafinga JKT Luteni Kanali Chalamila

















Kikundi cha Singe





































RC Hapi Akiwa katika Eneo la vikwazo














Mkuu wa Mkoa Iringa Mhe Ally Hapi Akiondoka Katika eneo la Viwanja vya Vikwazo katika Kikosi cha Jeshi Mafinga Baada ya Kumaliza zoezi la Ufungaji wa Mafunzo ambapo alikuwa Mgeni rasmi wa sherehe hizo na kujionea umahiri mkubwa wa Vijana wa JKT Mujibu wa Sheria 2018 katika nyanja mbalimbali.
Picha zote na Amani Mbwaga
Kwa Maoni au Ushauri Wasiliana nasi;
Mob: +255 656 632 566
E-mail Prof.mbwaga@gmail.com

No comments:

Post a Comment