Tuesday, September 4, 2018

DC Mufindi Afunga Kiwanda cha Wachina kwa siku 14

Mkuu wa Wilaya Mufindi akitoa tamko la kukifunga kiwanda cha Wachina cha Evergreen kwa Siku 14 Mafinga Mjini

Na Amani Mbwaga Mafinga- Iringa.
Ni baada ya mauaji ya mfanyakazi mmoja wa kiwanda hicho kuuwawa kutokana na kipigo kutoka kwa walinzi wawili ambao ni wamasai na Mchina mmoja katika eneo la Kinyanambo Mafinga Mjini, Wilayani Mufindi Mkoani Iringa.

Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri David William leo amefunga kiwanda cha Wachina kijulikanacho kama Evergreen kinachozalisha Siling Bodi kwa muda wa siku 14 kutokana na Kifo cha Mfanyakazi wa kiwanda hicho lakini pia kutokidhi kwa viwango vya ubora wa afya, mazingira na usalama kazini.

Mnamo tarehe 23 Agosti 2018 Marehemu bwana Omari Ibrahim Chokai aliyekuwa mfanyakazi wa kiwanda hicho cha Evergreen alifariki dunia baada ya kupokea kipigo hadi kufariki kutoka kwa Walinzi wa kampuni hiyo ambao mpaka sasa wanashikiliwa na Jeshi la  Polisi katika kituo cha Polisi Mafinga kwa ajili ya upelelezi zaidi wa tukio hilo.

Kwa mujibu wa ndugu wa marehemu inasemekana kwamba siku ya tukio Marehemu na wenzake walikua wakifanya service ya baadhi ya mashine ikiwemo kubadilisha oil ndipo marehemu alijaribu kuondoka na oil chafu na hapo ndio walinzi walimwita mwizi kwa kushirikiana na Mchina Mmoja kumpiga hadi mauti yalipomkuta huku wakifahamu fika kama marehemu huyo ni mfanyakazi wa kampuni hiyo.

Mmoja wa ndugu wa marehemu Bwana Selemani Boke aliwaambia waandishi wa habari kwamba baada ya kifo cha ndugu yao tarehe 24 Agosti 2018 walisafirisha mwili wa marehemu hadi Kondoa Irangi na kuuzika, baadae walienda polisi ili kufahamu kwa kina kuhusu kifo cha ndugu yao ili kuhakikisha kwamba haki inatendeka.

Bwana Boke alisema familiya imetumia zaidi ya Tsh Milioni 3 na laki 5 lakini uongozi wa kiwanda haujafanya lolote na kila walipokuwa wakiomba ushirikiano hawakupatiwa hata kidogo ndipo walipoamua kuandika barua kwa Mkuu wa Wilaya mufindi ili kuona jinsi gani anawasaidia ili haki yao ipatikane.

Mkuu wa Wilaya Mufindi baada ya kupata malalamiko hayo alianza kuyafanyia kazi na leo hii alifika kiwandani hapo akiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya.

Lakini pia alikuwa na  wataalamu mbalimbali kutoka NEMC, OSHA, Afisa Kazi Mkoa, Katibu wa Chama cha Wafanyakazi TUICO Mkoa wa Iringa na wataalamu wengine kutoka Halmashauri ya Mji Mafinga ambao walifanya ukaguzi wa kiwanda na kutoridhika na mazingira ya kiwanda hasa usalama kwa wafanyakazi na mazingira kutokuwa rafiki.

“Kwa kuzingatia sheria zote za kazi, usalama kazini na sheria ya mazingira kama wataalamu hawa walivyokwishafanya, Mimi Mkuu wa Wilaya Mufindi natamka na ninasema kiwanda kinasimama na nakifunga kwa siku 14 wawe wamerekebisha mapungufu yote yaliyoainishwa na wataalamu na pia ndani ya siku hizo wawe wamelipa gharama zote za kumsafirisha marehemu mpaka kwao Kondoa Irangi zinazofikia Milioni 3 na Laki 5”. Alisema Mhe Jamhuri.

Mkuu huyo wa Wilaya alisema kwa uchungu wasipotekeleza hayo waje hapa wang’oe mitambo yao na kuirudisha china, ni afadhali tubaki na unyonge wetu kuliko kunyanyaswa ndani ya nchi yetu iliyokwishapata uhuru haiwezekani.

Wakikamilisha yote hayo wafanyakazi wote wamehakikishiwa kurudi kazini na asisikie mtumishi hata mmoja anakatwa jina lake wote ni lazima warudi, “Ili mbegu iote ni lazima kwanza ife ndio inamea vizuri sasa tumeamua kufa kwa ajili ya maslahi mazuri mbele ya safari” Alisisitiza Mhe Jamhuri.

Alimaliza kwa kuwataka wafanyakazi kuchukua tamko hilo kama ni hatua nzuri ya kurekebisha hali ya kazi ili baada ya siku 14 mambo yawe mazuri.

Kwa upande wake Mratibu wa NEMC Nyanda za Juu Kusini Bwana Goodlove Mwamsojo alisema toka wamekipa kiwanda hicho cheti cha mazingira kwa ajili ya kuendesha shuguli zake hawajatekeleza shariti hata moja.

Hivyo kwa mujibu wa sheria ya mazingira ya mwaka 2004 mazingira ya kiwanda ni hatarishi, hawa  watu wanatishia usalama na afya za wafanyakazi hivyo wamestahili kupigwa faini ambayo haitapungua wala kuzidi Tsh Milioni 50.

“Sisi tutaendelea kufanya kazi wa mujibu wa sheria ya mazingira na kama kweli wana nia ya kuendeleza uchumi wa nchi hii ni lazima wajali afya za Watanzania” alisema Bwana Mwamsojo.

Kwa upande mwingine Msimamizi wa Ofisi ya Wakala wa usalama na Afya Ofisi ya Kanda nyanda za juu kusini Mbeya Injinia Faston Uswege alisema sisi kama OSHA tunasimamia sheria namba 5 ya mwaka 2005 ya uslama kazini.

“Watu wa OSHA Walipita mwezi wa 12 mwaka jana na wakatoa maelekezo ikiwemo kuwapatia vitendea kazi nya kiusalama na mpaka sasa halijatekelezwa” alisema Bwana Uswege.

Lakini pia suala la vyoo, kulingana na idadi ya wafanyakazi karibu 400 kutumia idadi ya matundu yaliyopo haiwezekani lakini pia vyoo havina hadhi ya kwenda kujisaidia na pia suala la maji ya kunywa yanayotumika hapa si safi na salama lakini mwajiri hajali hata kidogo.

Hatua imechukuliwa na OSHA kukitoza kiwanda hicho faini isiyopungua wala kuzidi Tsh Milioni 17 lakini pia ametakiwa atoe vitendea kazi kwa wafanyakazi wote ndani ya siku 14 alizopewa.

Aidha Afisa kazi Mkoa wa Iringa Bwana Daudi Samweli alisema kiwanda kimekuwa na manyanyaso na hakuna uongozi unaoeleweka kila mchina anayekuja ni Bosi.

“Kwa kufuata matakwa ya sheria ya kazi na miongozo mbalimbali ya kisera sisi tunawafikisha mahakamani viongozi wa kiwanda hiki ili watekeleze mambo tunayowaambia kila siku lakini pia wafanyakazi wenyewe hawana mikataba na hawataki kutoa, sasa hatutakubali kuona wafanyakazi wananyanyasika kwa namna yoyote ile" alisema Bwana Samweli.

Katibu wa chama cha wafanyakazi TUICO Mkoa wa Iringa  na Njombe Bwana Karim Bachalla kwa upande wake alisisitiza kwamba Wafanyakazi wanatakiwa kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi hii lakini pia nao wawekezaji wafanye kazi kwa kufuata sheria taratibu na matakwa ya nchi.  

HABARI PICHA
Mkuu wa Wilaya Mufindi (Katikati )akitoa maelekezo kwa Wachina Kushoto kwake ni Katibu wa TUICO Mkoa wa Iringa na Njombe Bwana Karim Bachalla 

Ukaguzi wa Kiwanda Ukiendelea

Mitambo ndani ya Kiwanda cha Evergreen

Wafanyakazi wakiendelea na kazi wakati wa ukaguzi



Majadiliano ya Wataalamu Mbalimbali wakiwa katika Ukaguzi wa Kiwanda cha Evergreen



Mratibu wa NEMC Nyanda za Juu Kusini Bwana Goodlove Mwamsojo (Kulia) akitoa maelezo kwa Mkuu wa Wilaya Mufindi baada ya kumaliza ukaguzi wa kiwanda


Msimamizi wa Ofisi ya Wakala wa Usalama na Afya OSHA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Mbeya  Injinia Faston Uswege akitoa mrejesho ya walichokiona baada ya kufanya ukaguzi ndani ya kiwanda cha Evergreen Mafinga Mjini.

Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri William Akiongea na Wafanyakazi na Wamiliki wa Kiwanda cha Evergreen kuelezea nia ya Kukifunga kutokana na kutokidhi vigezo.


Injinia Faston Uswege Kutoka OSHA Nyanda za Juu Kusini akitoa Tamko la Kukitoza Faini kiwanda cha evergreen kwa kwenda kinyume na sheria  na taratibu za Afya Mazingira na Usalama Kazini.



Afisa Kazi Mkoa wa Iringa Bwana Daud Samweli nae akieleza alichokibaini na hatua zitakazochukuliwa


Katibu wa chama cha wafanyakazi TUICO Mkoa wa Iringa  na Njombe Bwana Karim Bachalla kwa upande wake akisisitiza kwamba Wafanyakazi wanatakiwa kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi
Baadhi ya Wachina na Wafanyakazi wa Kiwanda hicho wakisikiliza kwa makini maelekezo ya serikali (Picha zote na Amani Mbwaga)
Kwa Maoni au Ushauri Wasiliana nasi:
Mob:+255 656 632 566
E-mail:prof.mbwaga@gmail.com

No comments:

Post a Comment