Friday, August 31, 2018

Naibu Waziri wa Kilimo Mhe Omary Mgumba Akipongeza Chama cha Ushirika wa Wakulima wa Chai Mkonge – Mufindi.

Naibu waziri wa Kilimo Mhe Omary Mgumba

Na Amani Mbwaga, Mufindi-Iringa
Naibu waziri wa Kilimo Mhe Omari Mgumba amekipongeza chama cha ushirika cha wakulima wa chai Mkonge baada ya kupata tuzo ya kuwa chama bora cha ushirika ngazi ya mkoa mwaka 2017 na mwaka huu 2018 kilipata tuzo ya mshindi ngazi ya taifa katika tasnia ya chai katika vyama vya msingi Tanzania.

Pongezi hizo zimetolewa na Naibu waziri wa kilimo alipokuwa katika ziara yake ya kikazi katika Kijiji cha Mkonge kata ya Luhanga Tarafa ya Ifwagi wilaya Mufindi Mkoani Iringa kwa lengo la kujionea shughuli za kilimo cha chai jinsi zinavyofanyika katika Wilaya ya Mufindi hususani kukutana na Wakulima kujua wanafursa gani changamoto, zipi na mikakati gani wanayo ili kusonga mbele katika kilimo chao.

Chama hiki kimesajiliwa kwa sheria ya nchi ya vyama vya ushirika mnamo tarehe 29 Aprili 2018 na kupewa hati Na IR 417, pia kimefanikiwa kutoa washindi wa ukulima bora kitaifa wa zao la chai, kikanda na kitaifa kwa miaka mitano mfululizo kuanzia mwaka 2008-2012.

“Niwapongeze sana kwa ushindi mkubwa wa mkoa kanda na kitaifa kwa kuwa chama bora cha msingi wa mazao na masoko Tanzania na mlipokuwa mnapewa nafasi hii na kuchukukua kombe nilikuwepo pale Mwanza kweli mnastahili na mwanzo nilikuwa sijawafahamu vizuri lakini kwa namna tu maonesho yenu yalivyokuwa yanaendelea kila mtu aliona kwamba mnastahili kupata ngao hizi” alisema Mhe Mgumba.

 Mhe. Mgumba aliendelea kusema kuwa wanawatia moyo na pia wanawatoa kimasomaso kama serikali na Wizara ya kilimo ambayo ushirika uko chini yao ambapo wengine hubeza uwepo wa ushirika lakini chama cha ushirika Mkonge wameonesha kwa vitendo.

Mafanikio ya Chama cha ushirika wa wakulima wa Chai Mkonge ni mengi sana lakini baadhi ni ongezeko la wanachama kutoka 174 mwaka 1971 hadi kufikia wanchama 652 waliopo sasa, Upanuzi wa Mashamba ya chai kutoka hekta 118 za mwaka 1971 kufikia hekta 344 zilizopo sasa, Uzalishaji wa majani mabichi ya chai umeongezeka kutoka kilo takribani laki 856,829 za mwaka 1971 na kufikia wastani wa kilo milioni 2 na zaidi za majani mabichi kwa mwaka.

Mchango wa taasisi na mashirika mbalimbali katika kuendeleza zao la chai katika ushirikwa wa Mkonge hawakuwa nyuma, ambapo Mkonge Tea Block Farm ilipata mkopo toka kwa wahisani wenye mashariti nafuu kutoka kwa shirika la Marekani African Development Foundation (ADF) kupitia shirika la CSDI Tanzania na kutoa mkopo wa Tsh. Milioni 271.9 kwa ajili ya kuimarisha na kuendeleza zao la chai katika Ushirika wa wakulima wa chai Mkonge Wilayani Mufindi.

Halmashauri ya Wilaya Mufindi kupitia DAPS ilisaidia kukamilisha miradi minne ambayo iliibuliwa na wanachama wenyewe ikiwemo ukarabati wa barabara ziendazo mashambani kilomita 6 yeye thamani ya Tsh Milioni 80, ujenzi wa mabanda10 kwenye vituo vya kupimia chai vyenye thamani ya Tsh milioni 22, ununuzi wa Powertiler 2 zenye thamani yaTsh Milioni 16 na mradi wa ufugaji kuku Tsh milioni 2.

Wakala wa maendeleo ya wakulima wadogo wa chai Tanzania (TASHTDA) ni miongoni mwa taasisi zilizochangia maendeleo ya chai Mkonge, wao walichangi fedha kiasi cha Tsh milioni 1 na mafuta Dizeli lita 100 kusaidia ujenzi wa ofisi.
Aidha bodi ya chai Tanzania (TBT) nao wapo bega kwa bega katika kutetea haki katika tasnia ya chai katika mikataba na matatizo yanapotokea kati ya ushirika na wanunuzi wa chai basi huingilia kati pia wamejenga banda moja la mfano kwa ajili ya kupimia chai.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri William alisema serikali imejitahidi kutafuta wafadhili na wadau mbalimbali ambapo tayari kuna uhakika wa kupata km 40 kutoka sawala hadi Lulanda ikiwa ni moja ya kupunguza changamoto ya miundombinu ya barabara.

Nae Diwani wa kata ya Luhanga Mhe Abeid Mhongole akitoa salamu zake kwa Naibu Waziri wa kilimo alisema wakulima wa chai katika eneo lake wamekuwa na changamoto nyingi ikiwemo bei ya mauzo ya majani mabichi ya chai kuwa ndogo, ingawa bei ya mauzo ya majani mabichi viwandani iliongezeka mwaka 2017 kutoka 250 kwa kilo hadi 287.11 pia mwaka 2018 kutoka 287.11 hadi 314.11 kwa kilo.


“Mheshimiwa Naibu Waziri bei ya kilo moja ya chai kwa sasa ni Tsh 314 lakini yeye huyu mkulima ni mmiliki wa shamba, analima kwa nguvu zake mwenyewe anagharamia mbolea pamoja na madawa lakini ukilinganisha na wenzetu wenye makampuni mfano UNLIVER mfanyakazi wa chai yeye analipwa Tsh 300 kwa kilo tofauti ya Tsh 14 tu ya mkulima wa chai hivyo unakuta huyu mkulima gharama za uzalishaji shambani kuwa kubwa na kumeza faida ya mkulima na kipato chake kuwa chini sana, hali hii inapelekea baadhi ya wakulima kutelekeza mashamba yao na kujihusisha na shughuli nyingine kama kusomba mbao ” alisema Mhe. Mhongole.

Akisoma risala Katibu wa Chama cha Ushirika Bwana Venusto France aliongeza kwamba Changamoto nyingine ni mkulima kutoshiriki katika mnyororo wa thamani katika zao la chai kwa kuishia kuuza majani mabichi pekee na bei kubwa ya pembejeo inayopatikana bila ruzuku ya serikali.

Akijibu changamoto ya bei Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya chai Tanzania Bwana Theophord Ndunguru alikiri changamoto hiyo na kusema kwamba tatizo hilo linatokana na mnada wa soko kuwa Mombasa Kenya hivyo wao kujipendelea lakini pia ubora  wa chai hivyo serikali tayari inamkakati wa kuanzisha mnada wake Jijini Dar es salaam ili kusaidia bei kupanda.

Kilimo cha chai Mkonge kilianzishwa mwaka 1971 chini ya mamlaka ya chai Tanzania (MACHATA) au TTA wakulima waanzilishi walikuwa 174 ambao walimiliki hekta 118.Chama kilianzishwa mwaka 1989 kama kikundi cha wakulima baada ya Mamlaka ya chai Tanzania (TTA) Kusitishwa.

Lengo la kuanzishwa kwa chama hiki lilikuwa ni kuwaunganisha wakulima wa chai Mkonge Katika kilimo cha zao la chai na kuwa na sauti moja katika kudai haki kutatua changamoto pamoja na kutafuta fursa.


HABARI PICHA
Naibu Waziri wa Kilimo Mhe Omary Mgumba akieleza lengo la ziara yake katika Ofisi za Mkuu wa Wilaya Mufindi

Naibu waziri wa Kimlimo Mhe Mgumba katikati, kulia kwake ni  Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mufindi Ndugu Yassin na kushoto kwa waziri ni Mkuu wa Wilaya Mufindi he Jamhuri William.


Chai inayolimwa Mufindi


Wataalamu mbalimbali na Wananchi wa kijiji cha Mkonge Wilayani Mufindi wakimsijiliza kwa makini Mhe Naibu Waziri wa Kilimo

Mkuu wa Wilaya Mufindi  Mhe William akitoa utambulisho kwa wananchi na wanachama wa ushirika wa wakulima wa chai mkonge kutokana na ugeni wa Naibu waziri wa Kilimo ,he Mgumba 


Mwenyekiti wa Ushirika wa Wakulima wa Chai Mkonge Bwana Sentino Mdena akiukaribisha ugeni wa Naibu waziri wa Kilimo.


Katibu wa Ushirika wa Wakulima wa Chai Mkonge bwana Venusto France akisoma taarifa ya ushirika kwa Naibu Waziri wa Kilimo


Naibu Waziri wa Kilimo akiongea na Wananchi na Wakulima wa Chai Katika Kijiji cha Mkonge Kata ya Luhanga Tarafa ya Ifwagi Wlayani Mufindi Mkoani Iringa.


Wananchi na Wakulima wa Chai wakiendelea kumsikiliza Mhe Mgumba Naibu Waziri wa Kilimo.
Picha Zote na Amani Mbwaga
Kwa Maoni au Ushauri Wasiliana nasi:
Mob: +255 656 632 566
E-mail:prof.mbwaga@gmail.com



Wednesday, August 29, 2018

Halmashauri ya Wilaya Mufindi yavuka lengo Ukusanyaji wa mapato na kufikia asilimia 90.96


Na Amani Mbwaga Mafinga.
Halmashauri ya Wilaya Mufindi Imevuka lengo la Ukusanyaji Mapato yatokanayo na vyanzo vya ndani katika mwaka wa fedha 2017/2018, na kufikia silimia 90.96.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe Festo Mgina wakati wa kutano wa Baraza la Madiwani la robo ya nne lililofanyika leo katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mkoani Iringa.

Ilielezwa kuwa katika kipindi cha Julai 2017 hadi Juni 2018 Halmashauri ilikusanya na kupokea jumla ya Tsh Bilioni 35.3 kati ya mapato hayo Tsh Bilioni 3.5 ni mapato yaliyotokana na vyanzo vya ndani, Tsh Bilioni 24.6 ni mishahara, Tsh bilioni 5 ni miradi ya maendeleo na Tsh Bilioni 2 ni matumizi ya kawaida.

Aidha katika kipindi cha Julai 2017 hadi Juni 2018 mchango wa wananchi katika kutekeleza miradi ya maendeleo ulikuwa na thamani ya Tsh Milioni 793.5.

Mlinganisho wa mapato halisi ya Tsh Bilioni 35.3 kwa kipindi cha Julai 2017 hadi Juni 2018 na makisio ya Tsh Bilioni 51.13 ya mwaka 2017/2018 unaonesha kuwa Halmashauri imekusanya asilimia 68.4 ya lengo la mwaka wa fedha wa 2017/2018.

Aidha mlinganisho wa mapato yatokanayo na vyanzo vya ndani yaliyokusanywa kwa kipindi cha Julai 2017 hadi Juni 2018 ya Tsh  Bilioni 3.5 na makisio ya mapato yanayotokana na vyanzo vya ndani ya Bilioni Tsh 3.8 kwa kipindi hicho yanaonesha kuwa Halmashauri ya Wilaya Mufindi imekusanya asilimia 90.96 ya lengo la mwaka.

“Mimi nawapongeza sana Mkurugenzi na timu yako kwa kufikia mafanikio Makubwa ya ukusanyaji mapato katika Halmasahuri yetu, niwasihi muendelee kufanya vizuri zaidi katika ukusanyaji lakini pia ni lazima tuongeze kasi na kuwa wabunifu wa kuwapata watu wakorofi wanaokwepa kulipa ushuru na kodi mbalimbali za serikali” alisema Mhe Mgina.

Aidha amewaasa Waheshimiwa Madiwani kushirikiana na kuendelea kujenga Mahusiano mazuri zaidi na Ofisi ya Mkurugenzi na wataalamu wake ili kuwaletea maendeleo wananchi wa Mufindi na Taifa kwa ujumla.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri David William aliwashukuru waheshimiwa madiwani kwa kuasidia utekelezaji wa majukumu ya serikali na hasa katika uhamasishaji wa kampeni ya ujenzi wa vyoo bora kwa wanachi.

Mhe Mwenyekiti tumezindua kampeni ya ujenzi wa vyoo bora kwenye wilaya yetu na haya ni maelekezo ya serikali, na sisi mufindi katika utekelezaji wa hilo tumejipa hadi tarehe 30 Oktoba 2018, tuhakikishe kila kaya inakuwa na choo bora. Alisema Mhe William.

Tafsiri ya choo bora tayari imekwishatolewa na wananchi wanaelewa, waheshimiwa madiwani wote wameombwa kuzungumza lugha moja, ili kuhakikisha wananchi wote wanakuwa na vyoo bora.

Utekelezaji wa kampeni hiyo unaambatana na usimamizi wa sheria ya mazingira.

Takribani asilimia 20% ya kaya ndio zenye vyoo bora Wilaya ya mufindi na asilimia 80% ni vyoo ambavyo si bora, kaya nyingi zinatumia vyoo vya asili sasa ni wakati wa kuhakikisha jamii inakuwa na vyoo bora.

Nae Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Bwana Isaya Mbenje amewakumbusha waheshimiwa madiwani kuhusu kulinda mali za asili na mazingira kwa ujumla kutokana Msimu wa kulimo unaokuja hivi karibuni ambapo watu wakati wa kuandaa mashamba huchoma moto hovyo unaoathiri mazingira na maliasili zilizopo.


“Katika Wilaya yetu tunatarajia msimu wa kilimo na tunaanza maandalizi ya mashamba kwa ajili ya kilimo hivyo tunaenda kuwa na kampeni ya kuhakikisha wananchi wanapoenda kusafisha mashamba yao wasichome na maeneo mengine” alisema Bwana Mbenje.

HABARI PICHA















Friday, August 24, 2018

Halmashauri ya Mji Mafinga Kununua Gari ya Taka.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga Mhe Charles Makoga akiongea na Wajumbe wakati wa Mkutano wa  Baraza la Madiwani uliofanyika leo hii katika ukumbi wa Halmashauri mjini Mafinga (Picha  na Amani Mbwaga)

Na Amani Mbwaga, Mafinga.
Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga limedhamiria kununua gari ya taka katika mwaka huu wa fedha ili kuongeza kasi ya ukusanyaji taka katika mji wa Mafinga na kuhakikisha mji unakuwa safi wakati wote.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga Mhe Charles Makoga katika Mkutano wa baraza la Madiwani wa Robo ya nne 2017/18 uliofanyika leo katika Ukumbi wa Halmashauri mjini Mafinga, Mkoani Iringa.

Tumenunua trekta jipya pia tuna gari nyingine kwa ajili ya kubeba taka lakini mwaka huu tunanunua gari nyingine ya taka kuhakikisha kwamba tunakuwa na magari ya kutosha kubebea taka katika mji wetu ili uwe safi zaidi na tutasimamia hapo” alisema Mhe Makoga.

Baraza limeagiza pia kila duka, taasisi za serikali na zile za binafsi kuhakikisha zinakuwa na vyombo vya kutunzia taka.

Agizo la Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri David William linawataka Wananchi wote kila Jumamosi ya Mwisho wa Mwezi kufanya usafi wa kina katika maeneo yote yanayowazunguka.

“Usafi ni jukumu la sisi wote hata Waheshimiwa Madiwani tunatakiwa kwenda kufanya usafi, basi kesho ni siku ya usafi tuungane wote kwenda kushiriki kufanya usafi katika Mji wetu wa Mafinga” alisema Mhe Makoga.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya  ambae pia ni Afisa Tarafa wa Tarafa ya Malangali Ndugu Daniel Dugange akitoa salamu za Mkuu wa wilaya amewataka watendaji kuja na mikakati bora zaidi ili kuboresha huduma bora kwa wananchi.

Amehimiza kudumisha ushirikiano zaidi katika kutatua changamoto mbalimbali ikiwemo migogoro ambayo viongozi wa ngazi ya kijiji, Kata na Tarafa imeshindikana ili kuwahudumia wananchi kwa ukaribu.

“Tukumbuke kwamba katika kutekeleza ilani ya CCM ya mwaka 2015 tumeshatafuna miezi 32 bado miezi 28 tu tumalize kipindi cha miaka 05, kwa hiyo tujipange vizuri tuwe na mpango mkakati mpango ambao unaangalia mambo 04, uwezo tulionao, udhaifu, fursa zilizopo na matatizo yaliyopo” Alisema Bwana Dugange.

Rasilimali ni chache lakini ni lazima kujipanga kwa uchache wa rasilimali zilizopo ili kuweza kufikia malengo na dira ya Taifa ya 2025.

Aidha Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga Bwana Voster Mgina amelieleza baraza la madiwani kuhusu ushirikiano ulioanza kufanywa baina ya shule za serikali na zile za binafsi ili kuongeza ufaulu katika Halmashauri ya mji Mafinga ukizingatia shule nyingi za binafsi katika mji huu zinafanya vizuri katika matokeo ya mitihani ya Taifa zaidi ya shule za serikali.

“Sasa hivi Waheshimiwa Madiwani tuna mitihani yetu ya Muhula ambapo tunatarajia kuwa na mtihani mmoja kwa shule zote za serikali na zile za binafsi hata hivi leo ninavyozungumza waalimu wetu wa shule zote wako shule ya Sekondari Bethel wakipitia mitahani ambayo itafanyika mwezi wa Novemba 2018 ni mtihani mmoja unatungwa na Waalimu wana upitia pale kuhakikisha unakuwa vizuri” alisema Bwana Mgina.

Aliongeza pia kumekuwa na mafunzo ya pamoja kwa waalimu wa shule zote za binafsi na serikali ambayo hufanyika mara kwa mara, na jana tu Baadhi ya waalimu wa Sayansi walikuwa wakipewa mafunzo ya vitendo katika sule ya Sekondari JJ Mungai kutoka kwa wakufunzi wa Chuo cha Kleruu ili kuwafundisha waalimu namna nzuri ya kuandaa masomo ya sayansi kwa vitendo.

Mkutano huu wa Baraza la Madiwani wa robo ya nne 2017/2018 umefanyika kwa mujibu wa sheria, kanuni za kudumu, na taratibu za uendeshaji wa serikali za mitaa.

HABARI PICHA

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga Mhe Charles Makoga akisisitiza Jambo.
Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya Mufindi, Afisa Tarafa ya Malangali Bwana Daniel Dugange akitoa salamu za Mkuu wa Wilaya katika Mkutano wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bwana Voster Mgina akitolea ufafanuzi jambo wakati wa Mkutano wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga 
Diwani wa Kata ya Boma Mhe Julist Kisoma akiuliza swali katika Mkutano wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga
Diwani Mhe Chesco Lyuvale akichangia katika moja ya agenda iliyokuwa inaendelea katika Mkutano wa Baraza la Madiwani
Diwani Mhe Denis Kutemile akiuliza swali wakati wa maswali ya papo kwa papo kwa Mwenyekiti wa Baraza la Madiwani  Halmashauri ya Mji Mafinga
Waheshimiwa Madiwani wakifuatilia kwa makini Mkutano wa Baraza la Madiwani wa Kwanza Kushoto ni Diwani wa kata ya Boma Mhe Damian Kyando naNyuma ni Wataalamu kutoka Ofisi ya Mkurugenzi Halmashauri ya Mji Mafinga.




Picha zote na Amani Mbwaga
Kwa Maoni au Ushauri Wasiliana nasi,
Mob:+255 656 632 566
E-mail:prof.mbwaga@gmail.com

Tuesday, August 21, 2018

Ziara ya Madiwani Kamati ya Fedha Uongozi na Mipango Halmashauri ya (W) Mufindi yakagua Miradi ya Maendeleo na Kuridhishwa nayo

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe Festo Mgina akipampu maji katika kisima kinachotumiwa na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mgalo Kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi na Diwani Kata ya Sadani Mhe Ashery Mtono (Picha na Amani Mbwaga)
Na Amani Mbwaga, Mufindi
Ziara ya Waheshimiwa Madiwani Kamati ya Fedha Uongozi na Mipango Ikiongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe Festo Mgina Kukagua Miradi ya Maendeleo ikiwa ni Robo ya Nne 2017/2018

Kamati Imetembelea na Kukagua Miradi ya Ujenzi wa Madarasa 02 na Ukarabati wa Madarasa 04 katika Shule ya Sekondari Igombavanu.

Imetembelea na Kukagua Lambo la Maji lililojengwa kutokana na Juhudi za Wanufaika wa Mfuko wa TASAF Ambaposasa linatumika katika Shughuli za Kilimocha Umwagiliaji na Unyweshaji Mifugo katika Kata ya Igombavanu.

Aidha Kamati iikagua Mradi wa Ujenzi wa Hosteli ya Wasichana katika Shule ya  Sekondari ya Mgalo iliyopo kata ya Sadani ambayo Mpaka sasa imejengwa kwa nguvu za Wananchi na Mbunge wao.

HABARI PICHA
Kamati ya Fedha Uongozi na Mipango Ikikagua Madarasa yaliyokarabatiwa na Serikali  tayari kwa matumizi ya Wanafunzi Katika Shule ya Sekondari Igombavanu


Madarasa  04 ya Shule ya Sekondari Igombavanu yaliyokarabatiwa na Serikali
Madarasa Mapya 02 yaliyojengwa na Serikali katika Shule ya Sekondari Igombavanu

Ukaguzi wa Choo cha Wanafunzi Kikikiwemo cha Walemavu Shule ya Sekondari Igombavanu


Lambo la Maji Lililopatikana kutokana na Juhudi za TASAF Ktika Kusaidia Kaya Masikini amblo linatumika katika Kilimo cha Umwagiliaji na Kunyweshea Mifugo Katika Kata ya Igombavanu
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mwenyesuti akipokea Malezo ya Mradi kutoka kwa Mwenyekiti wa Kijiji cha Igombavanu Katikakti ni Mratibu wa TASAF na Mwisho ni Makamu Mwenyekiti Halmashauri ya Wilaya Mufindi

 
Mwenyekiti wa Kijiji cha Igombavanu aliyeinama chini akionesha shamba la Matikiti Maji Yanayolimwa  kutokana na Umwagiliaji wa Lambo la Maji


Afisa Mtendaji Kata ya Sadani (Kulia) Bwana Romanus Nyigo akitoa Taarifa ya Mradi wa Ujenzi wa Hosteli ya Shule ya Sekondari Mgalo Mbele ya Kamati ya Fedha na Mipango

Kamati Ikikagua Ujenzi wa Hosteli ya Wasichana Iliyojengwa kwa Nguvu za Wananchi Katika Shule ya Sekondari Mgalo


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe Festo Mgina akipampu maji katika kisima kinachotumiwa na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mgalo Kulia kwake ni Afisa Elimu Sekondari Bwana John Lupenza


Picha zote na Amani Mbwaga

Mob:+255 656632566
E-mail:prof.mbwaga@gmail.com