Friday, August 24, 2018

Halmashauri ya Mji Mafinga Kununua Gari ya Taka.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga Mhe Charles Makoga akiongea na Wajumbe wakati wa Mkutano wa  Baraza la Madiwani uliofanyika leo hii katika ukumbi wa Halmashauri mjini Mafinga (Picha  na Amani Mbwaga)

Na Amani Mbwaga, Mafinga.
Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga limedhamiria kununua gari ya taka katika mwaka huu wa fedha ili kuongeza kasi ya ukusanyaji taka katika mji wa Mafinga na kuhakikisha mji unakuwa safi wakati wote.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga Mhe Charles Makoga katika Mkutano wa baraza la Madiwani wa Robo ya nne 2017/18 uliofanyika leo katika Ukumbi wa Halmashauri mjini Mafinga, Mkoani Iringa.

Tumenunua trekta jipya pia tuna gari nyingine kwa ajili ya kubeba taka lakini mwaka huu tunanunua gari nyingine ya taka kuhakikisha kwamba tunakuwa na magari ya kutosha kubebea taka katika mji wetu ili uwe safi zaidi na tutasimamia hapo” alisema Mhe Makoga.

Baraza limeagiza pia kila duka, taasisi za serikali na zile za binafsi kuhakikisha zinakuwa na vyombo vya kutunzia taka.

Agizo la Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri David William linawataka Wananchi wote kila Jumamosi ya Mwisho wa Mwezi kufanya usafi wa kina katika maeneo yote yanayowazunguka.

“Usafi ni jukumu la sisi wote hata Waheshimiwa Madiwani tunatakiwa kwenda kufanya usafi, basi kesho ni siku ya usafi tuungane wote kwenda kushiriki kufanya usafi katika Mji wetu wa Mafinga” alisema Mhe Makoga.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya  ambae pia ni Afisa Tarafa wa Tarafa ya Malangali Ndugu Daniel Dugange akitoa salamu za Mkuu wa wilaya amewataka watendaji kuja na mikakati bora zaidi ili kuboresha huduma bora kwa wananchi.

Amehimiza kudumisha ushirikiano zaidi katika kutatua changamoto mbalimbali ikiwemo migogoro ambayo viongozi wa ngazi ya kijiji, Kata na Tarafa imeshindikana ili kuwahudumia wananchi kwa ukaribu.

“Tukumbuke kwamba katika kutekeleza ilani ya CCM ya mwaka 2015 tumeshatafuna miezi 32 bado miezi 28 tu tumalize kipindi cha miaka 05, kwa hiyo tujipange vizuri tuwe na mpango mkakati mpango ambao unaangalia mambo 04, uwezo tulionao, udhaifu, fursa zilizopo na matatizo yaliyopo” Alisema Bwana Dugange.

Rasilimali ni chache lakini ni lazima kujipanga kwa uchache wa rasilimali zilizopo ili kuweza kufikia malengo na dira ya Taifa ya 2025.

Aidha Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga Bwana Voster Mgina amelieleza baraza la madiwani kuhusu ushirikiano ulioanza kufanywa baina ya shule za serikali na zile za binafsi ili kuongeza ufaulu katika Halmashauri ya mji Mafinga ukizingatia shule nyingi za binafsi katika mji huu zinafanya vizuri katika matokeo ya mitihani ya Taifa zaidi ya shule za serikali.

“Sasa hivi Waheshimiwa Madiwani tuna mitihani yetu ya Muhula ambapo tunatarajia kuwa na mtihani mmoja kwa shule zote za serikali na zile za binafsi hata hivi leo ninavyozungumza waalimu wetu wa shule zote wako shule ya Sekondari Bethel wakipitia mitahani ambayo itafanyika mwezi wa Novemba 2018 ni mtihani mmoja unatungwa na Waalimu wana upitia pale kuhakikisha unakuwa vizuri” alisema Bwana Mgina.

Aliongeza pia kumekuwa na mafunzo ya pamoja kwa waalimu wa shule zote za binafsi na serikali ambayo hufanyika mara kwa mara, na jana tu Baadhi ya waalimu wa Sayansi walikuwa wakipewa mafunzo ya vitendo katika sule ya Sekondari JJ Mungai kutoka kwa wakufunzi wa Chuo cha Kleruu ili kuwafundisha waalimu namna nzuri ya kuandaa masomo ya sayansi kwa vitendo.

Mkutano huu wa Baraza la Madiwani wa robo ya nne 2017/2018 umefanyika kwa mujibu wa sheria, kanuni za kudumu, na taratibu za uendeshaji wa serikali za mitaa.

HABARI PICHA

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga Mhe Charles Makoga akisisitiza Jambo.
Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya Mufindi, Afisa Tarafa ya Malangali Bwana Daniel Dugange akitoa salamu za Mkuu wa Wilaya katika Mkutano wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bwana Voster Mgina akitolea ufafanuzi jambo wakati wa Mkutano wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga 
Diwani wa Kata ya Boma Mhe Julist Kisoma akiuliza swali katika Mkutano wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Mji Mafinga
Diwani Mhe Chesco Lyuvale akichangia katika moja ya agenda iliyokuwa inaendelea katika Mkutano wa Baraza la Madiwani
Diwani Mhe Denis Kutemile akiuliza swali wakati wa maswali ya papo kwa papo kwa Mwenyekiti wa Baraza la Madiwani  Halmashauri ya Mji Mafinga
Waheshimiwa Madiwani wakifuatilia kwa makini Mkutano wa Baraza la Madiwani wa Kwanza Kushoto ni Diwani wa kata ya Boma Mhe Damian Kyando naNyuma ni Wataalamu kutoka Ofisi ya Mkurugenzi Halmashauri ya Mji Mafinga.




Picha zote na Amani Mbwaga
Kwa Maoni au Ushauri Wasiliana nasi,
Mob:+255 656 632 566
E-mail:prof.mbwaga@gmail.com

No comments:

Post a Comment