MAHAKAMA Kuu Kanda ya Mbeya, imebatilisha hukumu ya kifungo cha miaka 30 jela na viboko 12 aliyokuwa akiitumikia Mchungaji wa Kanisa la EAGT la Lwambi la mkoani Mbeya, Daniel Mwasumbi (57) aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya kumbaka na kumpa mimba mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Itende, Neema Beni (19), mkoani humo.
Aidha, Mchungaji Mwasumbi, alihukumiwa kifungo hicho, Januari 2, 2014 na Mahakama ya Wilaya ya Mbeya na Hakimu, Gilbert Ndeuruo, na serikali kuwakilishwa na wakili, Achiles Mulisa, ambapo Mahakama ilimtia hatiani kwa makosa hayo kinyume cha sheria kifungu cha 130 (2)e na 131(1) sura ya 16 ya sheria iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Mchungaji akitoka Mahakamani
Mchungaji wa Kanisa la Evangelical Assembles of God Tanzania (EAGT) la Lwambi la mkoani Mbeya, Daniel Mwasumbi,  akitoka Mahakamani baada ya kuachiliwa huru
Awali Mchungaji Mwasumbi alikuwa akitetewa na Wakili wa kujitegemea, Victor Mkumbe, ambapo ilidaiwa kutenda makosa hayo kati ya Januari 2008 hadi 2011 na kumpa ujauzito na kumzalisha mwanafunzi huyo watoto wawili wa kiume kwa nyakati tofauti na kumkatisha masomo kinyume cha sheria.
Rufaa
Katika upande wa rufaa iliyokatwa na Mchungaji huyo, alikuwa akitetewa na wakili akujitegemea, Benjamin Mwakagamba, wakati serikali iliwakilishwa na Wakili, Prosister Paul.
Akisoma hukumu hiyo leo Juni 4, 2014, Jaji wa Mahakama hiyo, Atuganile Ngwala, alisema sababu zilizowasilishwa kwenye Mahakama hiyo na wakili wa upande wa utetezi zilidhihirisha kuwa kulikuwa na ukiukwaji wa kisheria kwenye hukumu hiyo. Alisema katika utoaji wa hukumu hiyo haukuzingatia vipengele muhimu vya kisheria viilivyotumika na Mahakama ya Wilaya kumtia hatiani Mchungaji huyo.
Amebainisha kuwa kutokana na maelezo ya wakili, Mwakagamba, ni kuwa muda lilipotekea tukio hilo na liliporitiwa kwenye vyombo vya usalama unaonekana kuchelewa na kukinzana kwa baadhi ya vipengele,  lakini pia ushahidi ulitolewa mahakamani hapo na Mhanga ulionekana kujichanganya hivyo haujaonesha mrufani kutenda kosa hilo.
Hata hivyo, Jaji Ngwala alisema kuwa kwa upande wa Jamhuri ambayo ilikuwa ikiongozwa na wakili wa Serikali, Prosister Paul, una haki za kukata rufaa na kesi kuanza upya endapo utaona haujaridhika na hukumu hiyo.
Kwa upande wake wakili aliyekuwa akimtetea Mchungaji huyo, alisema rufaa ya mteja wake aliwasilisha sababu Saba za kupinga hukumu hiyo ambapo alidai kuwa hakimu wakati wa kutoa hukumu hiyo alikosea kisheria na haki kwa muda tukio hilo liliporipotiwa katika vyombo vya usalama.
SOURCE: Fikra Pevu.