Wednesday, November 28, 2018

Wizara ya Maliasili na Utalii Yanuia Kusomesha Wataalamu wa Ukuzaji wa Mbegu za Miti nchini


Na Amani Mbwaga.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Profesa Adolf Mkenda alipofanya ziara yake ya kwanza Wilayani Mufindi Mkoani Iringa  kuja kufanya kikao na Bodi ya programu ya Panda Miti Kibiashara (Private Forest Programme) inayofadhiliwa na Serikali ya Finland ambapo Mwenyekiti wake ni Katibu Mkuu wa wizara na Balozi wa Finland.

“Tumekubaliana kwamba tutahakikisha tunatenga fedha za kusomesha watanzania wenye taaluma hii ya ukuzaji miti (Tree Breeding) twende Sokoine pale watu wenye digrii ya kwanza ya misitu tuwafadhili waende wakasome digrii ya Uzamili (Masters) kwenye maeneo haya ikiwezekana tuwapeleke kwenye nchi ambazo zimebobea kama vile Finland illi wakirudi hapa waje hapa kutusaidia” alisema Prof. Mkenda

Prof Mkenda amebainisha kwamba pamoja na jitihada za kuwa na wakala wa mbegu za miti Tanzania(TTSA) bado kuna tabia ya kununua mbegu nyingi sana kutoka nje ya nchi na sababu ya kufanya hivyo ni kwamba ili upate mbegu bora ni lazima uwe na kitalu cha kuzalisha mbegu ili kuotesha miti ya majaribio na uwe na wataalamu.

“Naamini tunafursa kubwa ya kuwa wazalishaji wakubwa wa mbegu na kuziuza ndani na nje ya nchi lakini tuanataka kuamini kwamba program kama hii ya Panda miti kibiashara itakapoondoka tubaki na uwezo fulani wa kujiendeleza sisi wenyewe kwanza kwenye vijiji vyetu”,alisema Prof Mkenda

Aidha amesema walichokiona Mufindi kupitia shamba linalomilikiwa na kijiji la uzalishaji wa mbegu za miti  na mashamba  mengine kumilikiwa na wanakijiji wenyewe wamejifunza kitu kikubwa sana na kitaingia katika sera ya misitu ambayo inakamilishwa hivi karibuni wa ajili ya kuizindua mwakani.

Kabla ya kampeni ya Kitaifa ya kupanda miti vijijini                            (Village Afforestation Programme) kuanza rasmi mwaka 1970 kwa kiasi kikubwa jukumu la kupanda miti na kusimamia misitu lilikuwa la serikali kupitia idara ya misitu na nyuki mfano wa shamba la Miti Sao Hill, wakati wa kampeni hiyo wananchi na taasisi mbalimbali zilihusishwa na kuhimizwa kushiriki katika upandaji miti kwa ajili ya matumizi mbalimbali chini ya dhana ya misitu ya jamii (Community Forestry)

Kwa Upande wake Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri William ameishukuru sana serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais makini kwa kutoa muongozo mzuri mzuri sana kwa kushirikianana Panda miti kibiashara (PFP) Katika kutekeleza miradi mbalimbali ya kupanda miti.

“Tumeona katika maeneo mengi wameshirikiana na serikali katika mipango ya matumizi bora ya ardhi” alisema Mhe William.

Aidha Mshauri wa sekta binafsi ya misitu Tanzania Bwana Sangito Sumari amesema katika shamba la mbegu lililopo katika kijiji cha Holo ambalo lilianzishwa na program ya panda miti kibiashara chini ya ufadhili wa Serikali ya Finland kupitia wizara ya maliasili na utalii.

Shamba hilo limepandwa toka Januari 2015 na tayari limeshaanza kutoa matunda ambayo yataweza kuzalisha mbegu ambazo ni bora zitakazosaidia wakulima wa miti.

Madhumuni hasa ya Panda miti kibiashara ni kushughulika haswa na mnyororo mzima wa sekta ya misitu kuanzia mbegu bora, utunzaji wa misitu, uuzaji, uchakataji na utafutaji wa masoko ili kuwawezesha wakulima wa mazao ya miti ili wapate mbegu bora.

Mradi wa panda miti kibiashara (PFP) ulianza rasmi mwaka 2014 na kufikia Zaidi ya vijiji 59 lakini pia kupanda miti zaidi ya hekta 12000 na hizi zinajumuisha wakulima wadogo wadogo ambao wanafikia karibu ya wakulima 6000 ambao wanamiliki mashamba yao binafsi kupitia vikundi vyao alisema Bwana Sangito.

Takwimu zinaonesha kuwa eneo la misitu ya asili hapa Tanzania ni hekta 48,000,000 na misitu ya kupandwa ni hekta 553,000.

Kutokana na sera ya Taifa ya misitu ya mwaka 1998 sera ya Taifa ya hifadhi za mazingira ya mwaka 2004 na program mbalimbali za kuhamasisha upandaji miti kila mwaka, ni dhahiri kuwa serikali inahimiza wananchi na taasisi zishiriki kikamilifu katika suala la kupanda miti.

HABARI PICHA

Prof. Adolf Mkenda akiongea na Wanufaika wa Mradi wa Panda Miti Kibiashara katika Kijiji cha Lugolofu Wilayani Mufindi 
Balozi wa Finland Nchini Bwana Pekka Hukka

Kushoto Katibu Mkuu Wizra ya Maliasili na Utalii akisalimiana na Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri William


Dkt. Ezekiel Mwakalukwa Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki Wizara ya Maliasili na Utalii

Mshauri wa sekta binafsi ya misitu Tanzania Bwana Sangito Sumari


Kuelekea Mgololo Escarpment

Prof Mkenda akioneshwa ramani ya miradi inayotekeelezwa na Panda Miti Kibiashara








Mmoja wa wamiliki wa shamba la miti na Mnufaika wa mradi wa Panda Miti Kibiashara



Mtalamu wa Uandaaji wa mbegu katika Mradi waPanda mitiKibiashara Bwana Christopher Komakech akitoa maelezo ya kitalu cha shamba la kuotesha mbegu

Shamba la Kuandaa Mbegu za Miti Katika Kijiji cha Holo Wilayani Mufindi linalofadhiliwanamradi wa panda miti kibiashar huku likimilikiwa na Wanakijiji wa kijiji hicho



Prof Mkenda Kulia na Kushoto ni Mshauri wa Sekta binafsi ya misitu Tanzania Bwana Sumari wakiteta jambo. 




Prof. AdolfMkenda akisalimiana na Mwezeshaji wa Panda iti kibiashara wa kijiji cha Lugolofu Bwana Adolf  Ngilangwa




Bwana Ngilangwa Akisoma Taarifa ya Mradi





Mwenyekiti wa Kijiji cha Lugolofu akimweleza jambo Bwana Sumari




Prof. Mkenda akisalimana na Mwenyekiti wa Kijiji cha Lugolofu






Picha ya Pamoja (Picha zote na Amani Mbwaga)

No comments:

Post a Comment