Monday, July 16, 2018

Milioni 400 Kujenga, Kukarabati Kituo cha Afya Ifwagi Halmashauri ya Mufindi


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe Festo Mgina

Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi itatumia kiasi cha shilingi milioni 400 zilizotolewa na Ofisi ya Rais -TAMISEMI,  kujenga na kufanya ukarabati mkubwa wa kituo cha Afya Ifwagi kilichopo Kata ya Ifwagi ikiwa ni utekelezaji wa mpango mkakati wa Serikali unaokusudia kuiimarisha sekta ya Afya hususani Afya ya Mama na Mtoto katika Halmashauri ya  Mufindi. 

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Diwani wa kata ya Mninga Mhe. Festo Mgina, amesema, fedha hizo zitatumika kukarabati na kufanya utanuzi wa Wodi ya Wazazi, ujenzi wa jengo la upasuaji, ujenzi wa Nyumba ya Mganga sanjari na Jengo la Maabara.

Mhe. Mgina, amebainisha kuwa ujenzi na ukarabati huo, utatekelezwa kwa mfumo wa Force Account” ambapo Halmashauri hutumia Mafundi wenyeji watakao thibitishwa kuwa na weledi unaokubalika huku wakitakiwa kutekeleza jukumu hilo kwa kipindi kisichozidi miezi mitatu chini ya usimamizi wa karibu kutoka kwa Mhandisi wa ujenzi wa Halmashauri 

 “Nawahamasisha wananchi wote wa kata ya Ifwagi, kujitolea nguvu kazi wakati wa utekelezaji wa mradi huu muhimu kwa ustawi wa Afya zetu na Halmashauri ya Mufindi kwa ujumla” alisema Mhe.Mgina,

Aidha, ili kuhakikisha mradi huu unatekelezwa kwa wakati na ubora uliokusudiwa, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Profesa Riziki Shemdoe, akiwa ndiye mtendaji Mkuu, ameunda kamati maalum yenye vikosi kazi vitatu vinavyojumuisha Maofisa kutoka idara mbalimbali pamoja na wananchi ili kuhakikisha mradi huu unatekelezwa kwa wakati na  kuzingatia viwango elekezi.

Ikumbukwe kuwa mwishoni mwa mwaka jana Ofisi ya Rais -TAMISEMI ilitoa kiasi kama hicho cha fedha kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa kituo cha Afya Malangali kilichopo kata ya Malangali  na tayari ujenzi wake umekamilika na kinachosubiriwa ni mapokezi ya vifaa tiba  vyenye thamani ya shilingi Milioni 300 kutoka bohari ya dawa (MSD)

Chanzo Mufindi yetu Blog.

No comments:

Post a Comment