Sunday, January 13, 2019

UFAULU ELIMU MSINGI WAENDELEA KUSTAWI MUFINDI


Takwimu za ufaulu wa mitiahani ya kuhitimu elimu ya Msingi kwa Shule za Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi, zinaonesha kuendelea kupanda kwa kipindi cha miaka minne mfululizo kati ya mwaka 2015 - 2018 huku Halmashhauri ikiendelea kushika nafasi za kuridhisha Katika ushindani wa Kitaifa.

Hayo yamebainishwa na Ofisa mwenye dhamana ya taaluma wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Bi. Mariamu Ngalla, wakati akiwasilisha taarifa ya tathimini ya Mtihani wa kuhitimu Elimu ya Msingi kwa mwaka 2018 katika kikao maalum cha kila mwaka ambacho hutathimini na kuweka mikakati ya kufanya vizuri zaidi kwa mitini inayofuata.

Akiwasilisha mbele ya Mgeni wa heshima Mkuu wa Wilaya ya Mufindi  Mhe. Jamhuri William, Maofisa Elimu kata Waalimu Wakuu na Waalimu wa taaluma, ametanabaisha kuwa ufaulu umeendelea kupanda kutoka mwaka moja baada ya mwingine.

“Mwaka 2015 ufaulu wetu ulikuwa asilimia 84.4, mwaka 2016 ufaulu asilimia 84.9 tukishika nafasi ya 22 kitaifa kati ya Halmashauri 185, mwaka 2017 asilimia 84.37 tukishika nafasi ya 32 kitaifa kati ya Halmshauri 186, wakati mapema mwaka jana 2018 ufaulu umepanda kufikia asilimia 86.73 ambapo katika ushindani wa kitaifa tumeshika nafasi ya 35 kati ya Halmashauri 186. amesema

Akifafanua zaidi mafanikio ya mtihani wa mwaka 2018 Bi Ngalla, ameendelea kubainisha kuwa kati ya Shule kumi (10) zilizofanya vizuri kimkoa Halmshauri ya Mufindi imeingiza shule mbili (02) ambazo ni Ifwagi na Brooke Bond, lakini pia imeingiza Shule tano (05) kati ya Shule kumi (10) bora  za Serikali kwa ngazi ya Mkoa ambazo ni Shule ya Msingi Ifwagi, Mlimani, Nyanyembe, Kasanga na Makungu.

Akizungumza katika kikao hicho mgeni wa heshima Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Mhe. Jamhuri Willia, ameitaka idara ya Elimu Msingi kuongeza juhudi na mbinu za ufundishaji ili mtihani wa mwaka huu   waweze kufanya vizuri kwa kufaulisha kwa Zaidi ya asilimia 90 na kusisitiza kuwa mazingira na rasilimali za Mufindi ni rafiki kwa Watoto kusoma na kufaulu.

Halmshauri ya Wilaya ya Mufindi yenye jumla ya shule 146 ilishiriki katika mtihani wa mwaka jana 2018, ikiwa na watahiniwa 6,570 kati yao wavulana ni 3,053 na Wasichana 3,517 sawa na asilimia 99.8 ya watainiwa waliofanya mtihani.


Sehemu ya Maofisa Elimu kata, Walimu wa kuu na Walimu wa taaluma kutoka Shule 146 za Halmashauri.

No comments:

Post a Comment