Friday, January 4, 2019

DC Mufindi aongoza kikao cha kamati ya ushauri ya Wilaya Mufindi (DCC) na Kupitisha Mapendekezo ya Mpango wa bajeti ya mwaka 2019/2020.


Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe. Jamhuri William ameongoza kikao maalumu cha kamati ya ushauri ya Wilaya ya Mufindi kujadili kuridhia na kupitisha mapendekezo ya bajeti ya Halmashauri zote za Mji Mafinga na Wilaya Mufindi kwa mwaka wa fedha 2019/2020.

“Hiki ni kikao cha kawaida cha kamati ya Ushauri ya Wilaya ambacho kipo kisheria, serikali yetu ya wilaya mufindi chini ya Rais Wetu Dkt John Pombe Magufuli imetimiza miaka mitatu ya kuwepo madarakani na sisi kama wadau tumetimiza kwa njia moja au nyingine katika kuchangia pato la Taifa  kutokana na shughuli mbali mbali za kiuchumi na kutekeleza shughuli za  maendeleo ikiwemo utoaji wa elimu bure bila malipo afya, maji, kilimo, umeme, barabara na huduma nyingine nyingi za jamii”. Alisema Mhe. William

Kikao hicho kimefanyika kwa mujibu wa sheria ya fedha ya serikali za mitaa namba 9 ya mwaka 2013, Memoranda ya fedha ya serikali za mitaa (2009), agizo namba 15 (1) (a) (b) sheria ya bajeti Na. 11 Kifungu cha 21 ya mwaka 2015 na kanuni za Mikutano za Halmashauri ya Wilaya Mufindi na Mji Mafinga.

Kwa Mwaka 2019/2020 Halmashauri ya Wilaya Mufindi inatarajiwa kukusanya na kutumia fedha zaidi ya  jumla ya Tsh Bilioni 56.3 ambapo kiasi cha zaidi ya Tsh. Bilioni 39.1 ni Matumizi mengineyo kwa mchanganuo kwamba  mishahara ya Watumishi  ni zaidi ya  Bilioni 34.1 na Matumizi ya kawaida ni Bilioni 4.9.
Miradi ya Maendeleo itagharamiwa kiasi cha Tsh Bilioni 17.2 ambapo kati ya hizo, fedha za ndani ni Tsh Bilioni 8.7 na fedha za nje zitakuwa Bilioni 2.

Halmashauri kutokana na vyanzo vyake vya ndani inataraji kukusanya na kutumia jumla ya Tsh Bilioni  6.4 sawa na asilimia 14.4 ya bajeti yote, Mchango wa jamii kwenye Miradi ya  Maendeleo ni zaidi ya Bilioni 4.6 na Taasisi binafsi zinataraji kuchangia wastani wa Tsh Milioni 156.

Aidha Vipaumbele vya Halmashauri ya Wilaya Mufindi kwa mwaka 2019/2020 ni kuongeza upatikanaji wa huduma kwa kukamilisha miradi ya nyuma ambayo haikukamilika ikiwemo ya elimu na afya, ukarabati wa majengo ya baadhi ya shule za msingi, kuhimiza na kuongeza uzalishaji wa wa mazao ya kilimo na kuyaongezea thamani,  kuimarisha misingi ya utawala bora na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji mapato kwa njia ya kielekronic.

Kwa upande wake Halmashauri ya Mji Mafinga kwa mwaka wa fedha 2019/2020 imeomba kuidhinishiwa, kukusanya na kutumia zaidi ya kiasi cha Bilioni 25.5 kwa ajili ya matumizi mengineyo na miradi ya maendeleo.
Kiasi cha zaidi ya Sh. Bilioni 3.7 kimekadiriwa kukusanywa kutokana na na vyanzo mbalimbali vya Halmsahauri, Makisio haya ni zaidi ya Sh. Milioni 472.6 ambayo ni asilimia 14.22 ukilinganisha na makisio ya mwaka 2018/2019 ya zaidi ya Bilioni 3.3.

Aidha zaidi ya Bilioni 17.1 zinaombwa kuidhinishwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida kati ya fedha hizo kiasi cha Tsh Bilioni 13.8 ni kwa ajili ya mishahara na Tsh Bilioni 3.3 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo.

Katika Mwaka huu wa fedha 2019/2020 Halmashauri ya Mji Mafinga inataraji kukusanya na kutumia kiasi cha Bilioni 8.4 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo kutoka vyanzo mbalimbali ikiwemo Ruzuku kutoka serikali kuu ambayo ni zaidi ya Bilioni 5.4, Fedha za Wahisani zaidi ya Milioni 869 Mapato ya ndani asilimia 40% zaidi Bilioni 1.3,   nguvu za wananchi na wadau wa maendeleo Milioni 768.

Aidha Halmashauri hiyo imetaja vipaumbele vyake vikuu kuelekea Bajeti hii katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato ambapo ni  uanzishaji wa miradi ya kimkakati yenye lengo la kuongeza mapato ikiwemo, ujenzi wa stendi kuu ya mabasi, ujenzi wa maegesho ya magari ya mizigo, ujenzi wa soko la kisasa la mazao ya misitu, ujenzi wa miundombinu ya vitegea uchumi na biashara, lakini pia kuboresha mazingira ya uwekezaji na ujenzi wa viwanda na kuwekeza katika kilimo ikiwemo mradi wa shamba la matunda ya parachichi  na mradi wa umwagiliaji  Mtula.

Mapendekezo ya Bajeti ya mwaka 2019/2020 yameandaliwa kwa kuzingatia mambo yafuatayo, Muongozo wa Bajeti wa 2019/2020, Ilani ya Uchaguzi ya chama Tawala - Ccm ya 2015/2016 -2019/2020, Malengo ya Maendeleo endelevu (SDGs), Dira ya Taifa ya maendeleo 2025, Maelekezo ya Ki- Sekta na Mpango wa maendeleo wa miaka mitano na mipango mikakati ya Halmashauri pamoja na vipaumbele vya Taifa kama vilivyofafanuliwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli wakati wa kufunga bunge la 11 Mjini Dodoma.

Vilevie umezingatia Mwongozo wa Serikali wa kuandaa Mipango na Bajeti wa mwaka 2019/2020 uliotolewa na Wizara ya Fedha na Mipango mwezi Disemba 2018 ikiwa ni utekelezaji wa sheria ya Bajeti Namba 11 ya mwaka 2015 sehemu ya 21 na 22.

Kwa Mujibu wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bi. Saada Mwaruka na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Ndugu Isaya Mbenje wamebainisha kuwa Rasimu hiyo ya Mpango wa bajeti ya halmashauri hizo ni makadirio ya mapato na matumizi ya miradi ya maendeleo kwa mwaka 2019/2020 hivyo bado yanaendelea kujadiliwa na kupitiwa kwenye Baraza la wafanyakazi Mkoa, Ofisi ya Rais TAMISEMI pamoja na Wizara ya Fedha na Mipango.

Kwa hiyo maboresho yoyote yatakayotolewa yatajumuishwa ili kuboresha mpango na bajeti za Halmashauri hizo, vilevile marekebisho yataendelea kufanyika kutegemeana na ukomo wa bajeti utakaotolewa na serikali kwenye maeneo ya ruzuku.

HABARI PICHA
Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri Davidi William Mwenyekiti wa Kikao cha Ushauri cha Wilaya (DCC)

Mbunge wa Jimbo la Mufindi kusini Mhe. Menradi Kigola akichangia baadhi ya hoja katika kikao cha ushauri  DCC

Menyekiti wa Hamashauri ya Mji Mafinga Mhe. Charles Makoga

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe. Festo Mgina
Kaimu Mkurugenzi wa Hamashauri ya Wilaya Mufindi Bwana Isaya Mbenje


Bi Saada S. Mwaruka Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Mafinga
Kaimu Katibu Tawala Wilaya ya Mufindi (DAS)




Waliokaa mbele Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya Mufindi wakifuatilia kwa makini uwasilishwaji wa Rasimu ya bajeti ya mwaka 2019/2020
Baadhi ya wakuu wa Idara kutoka Halmashauri ya Wilaya Mufindiwakifuatilia kwa makini kikao hicho cha ushauri DCC
Waandishi wa Vikao








Mhandisi wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini TARULA Bwana Sanga akitoa Taarifa ya utekelezaji wa Matengenezo ya Barabara na Mpango wa Bajeti ya TARULA  2019/2020 Katika kikao cha ushauri cha Wilaya ya Mufindi




Diwani wa kata ya Sao Hill akichangia Moja ya Agenda


Afisa Tarafa wa Kasanga Bwana Dugange nae akichangia moja ya agenda ya TARULA

Afisa Mipango wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bwana Kyomo akisoma Rasimu ya Mpango wa Bajeti ya Halmashauri hiyo kwa mwaka wa fedha 2019/2020



Kaimu Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Bwana Quman akisoma Rasimu ya Mpango wa Bajeti ya Halmashauri hiyo kwa mwaka wa fedha 2019/2020
(Picha zote na Amani Mbwaga)

No comments:

Post a Comment