Tuesday, December 4, 2018

Wafanyabiashara Mufindi Watakiwa kutumia Fursa ya Mikopo Inayodhaminiwa na Benki Kuu BOT.

 Na Amani Mbwaga, Mufindi

WAFANYABIASHARA  Wilayani Mufindi wametakiwa kutumia kibiashara fursa ya mikopo inayodhaminiwa na Benki kuu ya Tanzania katika taasisi za kibenki   ili waweze kufanya biashara zenye tija ikiwa ni pamoja na kumuunga mkono Rais Magufuli katika dhana yake ya Tanzania ya viwanda.

Hayo yamesemwa Wilayani humo na Ofisa  mkuu  mwandamizi wa Benki kuu ya Tanzania (BOT) Bwana Sadiki Nyanzowa wakati akitoa mada ya Elimu kuhusu uwekezaji katika masoko ya fedha (Government Securities) kwa wafanyabiashara wilayani humo na kusema kuwa lengo la Benki kuu kudhamini ni kutaka wafanyabiashara na wajasiliamali waweze kukua na Kukopesheka ili waweze kuboresha biashara zao.

Alisema kuwa Serikali kwa kushirikiana na Benki kuu ilianzisha  mfuko wa udhamini  wa mikopo midogo na ya kati ili kukuza na kuendeleza  miradi hiyo  na kujenga mazingira ya kuwawezesha  wajasiliamali wenye miaradi midogo kupata  mitaji na  kuongeza  ukuzaji wa uchumi.

”Mfuko huu unalenga wajasiliamali wenye miradi midogo na ya kati  yenye mitaji  yakifedha  kati ya Milioni 5 hadi milioni 500,ambapo aombaji wanaweza  kutumia mfuko huu wa kudhamini kupitia mabenki na taasisi za kifedha zilizosajliwa  chini ya Sheria ya mabenki na Taasisi za fedha ya mwaka 2006”. Alisema

Alisema kuwa kuna sababu mbalimbali zinazozuwia wananchi kunufaika na fursa hii ikiwa ni pamoja na   utayari mdogo wa taasisi za  fedha kutoa huduma  ya mikopo kwa wakopaji wanaoanza biashara  kwa mara ya  kwanza  kwa sababu ya kukosa uzoefu.

Aiitaja sababu nyingine kuwa wakopaji wadogowadogo kutokuwa na uwezo  wa kuandaa mchanganuo wa biashara unaokubalika na tasisi za kifedha.

Kwa upande wake Meneja wa  Utawala wa Fedha Benki  kuu tawi la  Mbeya  Bakari Ally akizungumza alisema kuwa  Mafinga kuna fursa kubwa ya viwanda lakini bado wananchi na wafanyabiashara hawajapiga hatua kiuchumi hii ni kutokana na mitaji midogo.

Ally alisema kama anavyosema Mhe Rais Magufuli anataka wananchi wake wawe na raha kutokanana na furs zote zinazopelekea kubadilisha maisha yao, hivyo kupitia Benki kuu ipo kuwasaidia wananchi katika kufikia dhana ya uchumi wa viwanda kwa kusaidia kuongeza dhamana ya mikopo wanayoitaka katika mabenki.

”Sisi tumekuja Mafinga kwa Lengo la kuleta elimu hii ya dhamana ya serikali tukiona pia ni chagizo la kufanya wananchi waweze kuona fursa mbalimbali ambazo zipo sanjari na kuangalia namna bora ya kuwekeza katika biashara zetu ili mitaji iweze kupanuka na kufanya biashara zenye tija kwa manufa yetu na Taifa kwa ujumla” alisema Bwana Ally.

Nae Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Bwana Isaya Mbenje akifungua kikao hicho aliwataka wafanyabiashara kutumia kikao hicho kama fursa muhimu wa kujifunza namna ya kupiga hatua katika uwekezaji.

Aidha mmoja wa washiriki wa semina hiyo Bwana Henry Mangenya ambae pia ni Mwenyekiti wa TCCIA Wilaya Mufindi ameishukuru benki kuu kwa kuleta elimu hiyo ya kuhusu uwekezaji katika masoko ya fedha kwani wengi wao walikua hawajaipata ipasavyo kwani walikuwa na dhana ya uwekezaji kwenye masoko ni matajiri wakubwa tu lakini kumbe hata watu wa kawaida wanaweza kuwekeza aidha  ameiomba benki kuu kuendelea kutoa eimu hiyo nchi nzima.

Chimbuko la mifuko ya udhamini wa mikopo inayosimamiwa na benki kuu ilifanya mageuzi katika sekta ya fedha ya mwaka 1991 na kujenga mazingira bora ya soko huria na kuboresha huduma za kifedha nchini, hata hivyo upatikanaji wa mikopo hasa kwenye sekta ya kilimo na kwa wajasiriamali  wadogo na wa kati  (SME) ilibaki kama changamoto.


HABARI PICHA
  Meneja Utawala wa Fedha Benki  kuu tawi la  Mbeya Bwana Bakari Ally akizungumza na wafanyabiashara na wajasiriamali wa Wilaya ya Mufindi
Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya Mufindi Bwana Isaya Mbenje akifungua rasmi semina hiyo inayoendeshwa na BOT Katika ukumbi wa Halmshauri ya (W) Mufindi
Baadhi ya Wafanyabiashara na Wajasiriamali wakifuatialia kwa makini semina inayotolewa na Benki Kuu BOT
 Ofisa Mkuu  mwandamizi wa Benki kuu ya Tanzania (BOT) Bwana Sadiki Nyanzowa akitoa mada ya Elimu kuhusu uwekezaji katika masoko ya fedha (Government Securities) Wiayani Mufindi.





 


 



Mmoja wa washiriki katika semina ya BOT Iliyofanyika Mufindi akiuliza swali
Bi. Eudosia Mwidete Kutoka Benki kuu ya Tanzania ambae pia ni Mtoa mada ya Pili Katika semina ya wajasiriamali na wafanyabiashara iliyofanyika Wilayani Mufindi mapema leo.


 
Bi. Marry Mkwama Kutoka Benki Kuu Tanzania BOT Akisisitiza jambo katika semina ya wafanyabiashara na wajasiriamali iliyofanyika mapema leo katika ukumbi wa Halmsahuri ya Wilaya Mufindi

(Picha zote na Amani Mbwaga)

No comments:

Post a Comment