Tuesday, December 18, 2018

DC Mufindi Awafunda Wasimamizi wa Elimu Kuelekea Mwaka Mpya wa Masomo 2019.

Na Amani Mbwaga,

DC Mufindi Mhe Jamhuri William
Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe. Jamhuri William amewataka viongozi wanaosimamia elimu katika Halmashauri ya Wilaya Mufindi kuwa na mpango mkakati kabambe wa kuhakikisha wazazi wanatimiza wajibu wao katika mahitaji ya wanafunzi na kuagiza kuwa katika mwaka mpya wa masomo unaoanza mwezi Januari 2019 ni lazima mtoto aende shule hata kama ameshindwa kupata sare za shule.

Hayo yamesemwa wakati wa mkutano wa wazi wa mapitio, upimaji na utendaji kazi kwa Waalimu na viongozi wa elimu katika Halmashauri ya Wilaya Mufindi ikiwa ni kuelekea Maandalizi ya mwaka mpya wa masomo 2019.

Mhe. William alisema kikao hicho ni cha kazi, ambacho lengo lake kubwa ni kutoa maelekezo kwa lengo la kufanya utekelezaji sahihi, makini na wenye tija katika muhula mpya na mwaka mpya wa masomo wa 2019.
Aidha amethibitisha kwamba katika muhula wa kwanza wa mwaka mpya 2019 Halmashauri ya Wilaya Mufindi inategemea kupokea jumla ya wanafunzi 5,698 wakiwamo wavulana 2,599 na wasichana 3,099 ambao wamefaulu na kuchagulia kujiunga na kidato cha kwanza.

“Hivyo ni lazima tujipange kuhakikisha kila mwanafunzi aliyefaulu na kuchaguliwa anaingia kidato cha kwanza , hii ni pamoja na kutoa elimu bora ili kuinua kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa kidato cha pili, nne na sita kufikia zaidi ya asilimia 90 kwa mwaka ujao wa 2019” Alisema.

Serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi shupavu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli inatekeleza sera ya Elimu bure kuanzia darasa la awali mpaka kidato cha nne, lengo kuu la sera, ilani na maagizo ya viongozi wa kitaifa ni kuhakikisha watoto wote wa Tanzania wanapata elimu msingi bila kikwazo chochote hususani katika kufuta ada na michango yote ambayo ilionekana kuwa kero na kikwazo cha baadhi ya watoto wa kitanzania katika kupata elimu msingi.

Kwa mujibu wa barua ya Katibu Mkuu wa TAMISEMI Kumb.NaDC.297/507.01.146 ya tarehe 23 Novemba 2015 inayohusu mwongozo wa fomu ya kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za sekondari za serikali inasema “Elimu msingi bila malipo maana yake ni kwamba michango yote iliyokuwa inatozwa shuleni kutoka kwa wazazi/walezi imefutwa, sababu ya kufuta ada na michango hiyo ni kuimarisha uandikishaji, mahudhuriao na kuondoa vikwazo kwa wanaoacha shule kwa kushindwa kulipa ada na michango iliyokuwa inatozwa”.

Hata hivyo Mhe Wiliam amesisitiza kwamba maelekezo ya elimu bure hayana tafsiri ya kuathiri moyo wa kujitolea kwa wanajamii, wazazi na wadau mbalimbali, pale wanapoamua kuunga mkono juhudi za serikali yao kwa kuchangia michango mbalimbali wasivunjwe moyo.

Akitoa hali halisi ya elimu Afisa Elimu Sekondari Mwl. Mussa Ally amesema Halmashauri ya Wilaya Mufindi imekuwa ikiimarisha hali ya utoaji taaluma mwaka hadi mwaka, ambapo kwa matokeo ya kumaliza elimu ya msingi mwaka 2017 matokeo yalikuwa ni mazuri na jumla ya asilimia 84.26 ya wanafunzi walifanya vizuri na mwaka huu 2018 watoto wameendelea kuongeza ufaulu ambapo umefikia asilimia 86.73.

Ufaulu wa kidato cha pili kwa miaka 03 mfululizo 2015 hadi 2017 umekuwa wa wastani wa asilimia 89, kidato cha nne ulikuwa wastani wa asilimia 77 na kidato cha sita imekuwa ni wastani wa asilimia 99  na ukiangalia maelekezo ya serikali  kutoka BRN  ni asilimia 85.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati ya Elimu, Afya na Maji (Huduma za Jamii) Mhe. Flavian Mpanda amesema ufaulu wa sasa ukiangalia shule 10 zilizofanya vizuri Halmashauri ya Wilaya Mufindi ni mojawapo kwani imeingiza shule tano bora, na waliofanya kazi hiyo kubwa ni waalimu mbele yako nawapongeza sana na matokeo haya ni kutokana na umoja uliopo baina ya waalimu hawa na uongozi wa Halmashauri”

HABARI PICHA

Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe Jamhuri William


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe. Festo Mgina


Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Bwana Isaya Mbenje.


Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma za Jamii Mhe.Flaviana Mpanda


Afisa Elimu Sekondari (W) Mufindi Mwl. Mussa Ally


Mwenyekiti wa CWT (W) Mufindi Bwana Justine C. Kinyaga


Mwenyekiti TAHOSA Mufindi akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wakuu wa shule





Mkuu wa Wilaya Mufindi akisalimiana na Afisa Tarafa wa Kibengu Bi. Scolastica Rocky

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mufindi Mhe Festo Mgina akisalimiana na Afisa Elimu Sekondari (W) Mufindi Mwl.Mussa Ally.





DC Mufindi Kushoto akisalimiana na Mwakilishi wa Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mufindi


Afisa Elimu Sekondari Mwl. Mussa Ally akitoa taarifa ya hali ya elimu Halmashauri ya Wilaya Mufindi.


Afisa Elimu Sekondari Mwl. Mussa Alyy Akisalimiana na  Mkuu wa Dawati la Jinsia Wilaya ya Mufindi Inspekta Marry Haule

Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya Mufindi  Bwana Isaya Mbenje akiongea na wataalamu wa Elimu 




Picha ya Pamoja Mgeni rasmi na Meza Kuu


Picha ya Pamoja na Mgeni Rasmi na Maafisa Watendaji Kata


Picha ya pamoja na Maafisa Elimu Kata

Picha ya Pamoja na Wakuu wa Shule za Sekondari


Picha ya Pamoja na wakuu wa shule za Msingi




(Picha zote na Amani Mbwaga)
Mob:+255 656 632 566
E-mail: prof.mbwaga@gmail.com

No comments:

Post a Comment