Friday, July 5, 2019

Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Bashungwa Afanya ziara katika Viwanda vya nguo na Kutatua kero zao


Na Amani Mbwaga, Dar es salaam
Waziri wa viwanda na Biashara nchini Tanzania Mhe. Innocent Bashungwa Mapema leo hii amefanya ziara katika viwanda vya nguo kikiwemo cha NIDA na kile cha NAMERA vya jijini Dar es salaam.

Akiongea mara baada ya kutembelea viwanda hivyo Mhe. Bashungwa amesema lengo la ziara hiyo ni kupita katika viwanda vyote vya nguo nchini kujua changamoto zao na kisha serikali kuzifanyia kazi na hatimae kuwa na uzalishaji endelevu wa zao la  pamba na kuwanufaisha wakulima.

“Mimi nimekuja hapa kwa ziara mahususi, Wakulima wetu wa pamba wamehamasika sana kulima pamba, Msimu huu wa mwaka 2019 tunategemea kuvuna  zaidi ya Tani Laki 4 za pamba  kutoka tani Laki 220,000 za mwaka jana kwa hiyo tuna pamba za kutosha” alisema  Mhe. Bashungwa.

Aidha amesisitiza kwamba wakulima kwa upande wao wametimiza wajibu wao hivyo ni jukumu la Serikali kupitia wizara ya viwanda na biashara kuwatafutia masoko yenye tija.

“Kwa muda mrefu soko la pamba limekuwa likitegemea mlango mmoja tu, wakati wa enzi za Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere kulikuwa na viwanda vingi vya nguo na vilikuwa vinafanya kazi ipasavyo na kama vyote vingekuwepo basi kusingekuwepo na changamoto ya masoko katika zao la pamba hivyo ni wakati sasa wa viwanda vilivyopo na vitakavyojengwa kuhakikisha vinafanya kazi ipasavyo na Kuongeza Uzalishaji mara mbili zaidi  ili kuendana na kasi ya sasa ya Tanzania ya Viwanda".

Nchi ikifanikiwa kuchakata kila zao na kuliongezea thamani basi itakua ni chachu ya ongezeko la ajira hapa nchini na hatimae kukuza uchumi wa  taifa na wananchi kwa ujumla.

Dira kuu ya Wizara ya Viwanda na Biashara  ni "Kuwa na msingi shindani wa viwanda, mazingira bora ya uwekezaji na ukuaji wa biashara unaowezesha kukua kwa uchumi shirikishi na endelevu."

Waziri Bashungwa ataendelea na ziara hiyo nchi nzima baada ya Kuanza na Mkoa wa Kilimanjaro hapo jana na leo hapa Jijini Dar es salaam.


MATUKIO KATIKA PICHA
Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Innocent Bashungwa akiangalia Bidhaa zinazotengenezwa na Kiwanda cha Nguo NIDA Wakati wa ziara yake.
Mhe.Waziri Bashungwa wakati wa Majumuisho ya ziara

Pamba ikiwa katika Hatua za awali za uchakataji

Waziri wa Viwanda na Biashara (Katikati) akipokea maelezo ya namna Pamba inavyoanza kuchakatwa katika hatua za awali




Shughuli za Uzalishaji Kiwandani zikiendelea






Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Innocent Bashungwa (Kulia) akimsikiliza kwa Makini Mkurugenzi Mkuu wa Kiwanda cha Nguo NIDA na NAMERA  (Picha zote na Amani Mbwaga)

No comments:

Post a Comment