Friday, February 1, 2019

Halmashauri ya Mji Mafinga Yazindua Kampeni ya Upandaji Miti Katika Vyanzo vya Maji.


Na Amani Mbwaga, Mafinga.
Halmshauri ya Mji Mafinga jana imezindua kampeni ya upandaji miti aina ya Mivengi katika chanzo cha maji eneo la Makamadolesi kata ya Changarawe Wilayani Mufindi Mkoani Iringa, uzinduzi huo umeoongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mhe. Charles Makoga akimwakilisha Mgeni Rasmi Mkuu wa Wilaya Mufindi Mhe. Jamhuri William.

Kwa kuzingatia mabadiliko ya tabia ya nchi yanayosababaishwa na shughuli za kibinadamu za uvunnaji wa mazao ya misitu na kilimo kisichofuata hifadhi ya mazingira na vyanzo vya maji serikali iliamua kutenga tarehe mosi Aprili ya kila mwaka kuwa siku maalumu ya upandaji miti kitaifa.

Kampeni hiyo mwaka huu inaenda na kaulimbiu ya “Panda miti hifadhi Mazingira na Vyazo vya maji kwa vizazi vya sasa na vya baadae”

Hata hivyo kwa kuzingatia tofauti ya majira ya misimu ya mvua kuanza na kuisha katika maeneo haya, Mkoa wa Iringa ulipanga uzinduzi wa upandaji wa miti katika maeneo yote ya mkoa kufanyika mwezi Januari kila mwaka.

“Leo hii ni siku muhimu kwetu kwani inaelenga kukumbushana na kuelimishana juu ya umuhimu wa kuhifadhi na kutunza mazingira kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo” alisema Mhe. Makoga.

Ameendelea kusisitiza kwamba uhaba wa upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa mijini na vijijini aidha uharibifu wa vyanzo vya maji ni kero kubwa, na mfumo wa maji ni miongoni mwa  changamoto za mazingira zinazoendelea kulikumba taifa .

Pamoja na juhudi zinazochukuliwa na serikali katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira ni muhimu ifahamike kwamba mazingira ni sehemu ya maisha ya binadamu na ndio uhai wa viumbe, Maisha ya binadamu yanategemea ardhi, maji, mimea na hewa.

“Takwimu za hivi karibuni za sensa ya miti zinaonesha wazi kwamba idadi inapungua sana takribani hekta zaidi ya 270,000 hadi 300,000 zinapungua kutokana na ukataji miti hovyo na uchomaji mkaa” alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bi. Saada Mwaruka alisema Halmashauri yake imeandaa jumla ya miche 15,039 ambapo miche 5,000 ni pine na miche 5200 ni miti rafiki na maji (Mivengi), miche ya matunda parachichi 1,118, miche ya mapambo na vivuli 1400.

“Lengo la kupanda miche ya aina hii ni kwa ajili ya kuhifadhi mazingira kupendezesha maeneo ya wazi kuhifadhi vyanzo vya maji na kuimarisha mipaka ya maeneo mbalimbali” alisema.

Akisoma taarifa ya uzinduzi kwa mgeni rasmi Afisa Mazingira wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bwana Charles Tuyi alisema halmashauri hiyo imefanikiwa sana kwa upandaji wa miti kutokana na kuwa katika ukanda unaokubali mazao ya kilimo cha miti wananchi wake wanazidi kuhamasika kwani kila mwaka kwani  takwimu za upandaji  zimekuwa  zikizidi kuongezeka.

Licha ya mafanikio hayo Halmashauri hiyo bado inakumbwa na changamoto lukuki katika uhifadhi wa mazingira ikiwemo kuendelea kutokea kwa matukio ya moto kichaa unaoathiri misitu ya asili na ile ya kupandwa, uvamizi wa misitu na vyanzo vya maji kutokana na shughuli za kibinadamu, kukosekana takwimu halisi za miti iliyovunwa hasa miti michanga, uhaba wa wataalamu na vijiji vingi kutokuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi inayopelekea migogoro ya ardhi kutokea.

Bwana Tuyi ameeleza kwamba kutokana na changamoto hizo Halmashauri ya Mji Mafinga imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuwa na kampeni ya utoaji elimu juu ya udhibiti mioto jamii kwa kushirikiana na wakala wa huduma za misitu Tanzania TFS-Shamba la Miti Sao Hill ambapo kila mwaka elimu hiyo hutolea na kuunda vikosi maalumu vya kudhibiti moto.

Mbali na hayo Halmashauri imeendelea kusimamia sheria ndogo za mazingira, kushawishi wizara ya maliasili na utalii kuimarisha na kusimamia matumizi ya mfumo wa viwango (Standards) sahihi katika biashara ya mazao ya misitu ili kudhibiti uvunaji holela wa miti michanga.

Kwa upande wake Afisa Misitu wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bwana Peter Kibona amesema lengo kuu la halmashauri hiyo kwa mwaka 2019 ni kuotesha miche Milioni 1 na laki tano, hadi sasa zaidi  ya miche milioni 1 imepandwa katika maeneo mbalimbali na upandaji bado unaendeelea.

Kwa kipindi cha mwaka 2016 hadi sasa Halmashauri ya Mji Mafinga imepanda zaidi ya hekta 8,652.1 za miti.


Aidha Halmashauri hiyo imeanzisha vitalu vya miti ya aina mbalimbali ili kuweza kuhudumia wananchi kwa kuwagawia miti bure ili kuwapatia motisha katika upandaji  miti na uendelezaji wa miti hiyo kwa ajili ya  mazao ya misitu kwa faida ya vizazi vya sasa na baadae.

No comments:

Post a Comment